top of page
  • C-Sema Team

#116Stories: Kumpiga mtoto sio kumuadabisha!

Hivi juzi Kati, tulipokea simu kutoka kwa mama mmoja aliyetaka ushauri juu ya tabia ya mme wake kumpiga mtoto wao Ana mwenye umri wa miaka 12.

Kwa sababu hii Ana anamkwepa baba yake na kukaa nje ya nyumba mpaka baba yake atakapolala ndio yeye aingie ndani.

Mama huyo aliendelea kutueleza kuwa mumewe amekuwa mkali sana kwa Ana kuliko wadogo zake akimchapa mara kwa mara akidai kuwa kwa sababu Ana ni mtoto wa kwanza kwahiyo lazima awe na adabu.


“Kila nikijaribu kuingilia ama kuzungumza nae anakasirika sana na huondoka” alieleza Mama Ana.

Baada ya mazungumzo haya mshauri wetu alimpongeza kwa kufanya jambo sahihi kwa kutoa taarifa mapema.

Kesi ilipelekwa kwa Afisa Ustawi wa Jamii-Wilaya ambaye alifanya jitihada za kukutana na wazazi katika ofisi za serikali ya mtaa ambapo aligundua kuwa Baba yake Ana hakuwa akijua athari za matendo yake kwa mwanae na alikua akifanya kile alichofanyiwa yeye alivyokua mtoto.

Afisa Ustawi alimwelezea mbinu bora za malezi na uadabishaji bila kumvunjia mtoto haki zake na kumuumiza kwa adhabu kali. Pia, alielezwa namna bora za kuwasiliana na mke na watoto wake ili kutatua migogoro ya kifamilia kwa amani. Baba aliomba msamaha kwa binti yake na kuahidi kubadilika. Familia imeachwa chini ya uangalizi wa Serikali ya Mtaa wakiyatekeleza yale waliyoshauriwa na Afisa Ustawi. Ni muhimu kwetu sote kupinga adhabu kali kwa watoto kuanzia ngazi ya nyumbani. #SioLazima kumpiga mtoto kumuadabisha, tutafakari na kujielimisha njia njema za kulea watoto wetu.


Kwa maoni na ushauri tupigie simu namba 116 ambayo ni maalumu kwa huduma za mtoto nchini. Huduma hii haitozi malipo toka mitandao yote nchini. Vilevile unaweza kutupata kupitia ukurasa wetu wa Facebook: Sema Tanzania; Twitter: @SemaTanzania na www.sematanzania.org


4 views

Comments


bottom of page